Hesperian Health Guides

Baadhi ya magonjwa ambayo yanahusiana na kinyesi

Katika sura hii:

Magonjwa yanayohusiana na kinyesi ni pamoja na ugonjwa wa kuhara, Kipindupindu, minyoo ya safura, homa ya matumbo (taifodi), na amiba.

Kipindupindu

Kipindupindu ni ugonjwa hatari unaosababishwa na maambukizi ya vimelea viitwavyo kwa lugha ya kitaalamu vibrio cholerae ambao huambatana na kuharisha na kutapika sana.

Vimelea hivi hushambulia matumbo ya binadamu na baada ya siku moja hadi tano huanza kutoa sumu ambayo husababisha mharo mkali wenye maji mengi, kama maji yaliyooshea mchele. Baadhi ya wagonjwa pia hutapika sana, hali ambayo husababisha mtu kupoteza maji mengi kutoka mwilini. Asipotibiwa haraka hufariki katika saa chache.

Sw EHB Ch7 page 142-1.png

Dalili za kipidupindu

  1. Kuharisha kukiwa na maji mengi yenye rangi ya kijivu au rangi ya maji yaliyotumika kuoshea mchele.
  2. Kutapika sana
  3. Kuishiwa maji mwilini, ambapo dalili zake ni:
    • Kusikia kiu
    • Kujisiki mchovu na kuudhika kirahisi, na
    • Ngozi ya mwili inapovutwa hurudia hali yake ya kawaida polepole.

Asilimia 90 ya watu walioambukizwa vimelea vinavyosababisha kipindupindu hawaonyeshi dalili kali za ugonjwa huu. Wakati mwingine huharisha kidogo tu. Hali hii inadhihirisha umuhimu wa kuzingatia masharti ya afya daima kama njia kuu ya kujikinga.

Minyoo ya safura

Minyoo ya safura huambukiza matumbo ya binadamu na kawaida husababisha kuharisha au tumbo kufunga, maumivu ya tumbo, na kupungukiwa na hamu ya kula. Minyoo ya safura huenezwa kupitia mayai yake katika kinyesi cha mtu aliyeambukizwa. Baada ya kujisaidia nje ya choo, mayai ya minyoo hiyo huweza kuingia ardhini na kwenye kinyesi kingine.

Njia kuu za maambukizi ya minyoo ya safura ni pamoja na:

  • Kutembea bila kuvaa viatu na hivyo kukanyaga mayai ya minyoo hiyo kwenye udongo au kinyesi, ambapo minyoo hiyo hupata fursa ya kupenya kwenye mwili wa binadamu.
  • Kumeza udongo uliochafuliwa na mayai ya ugonjwa huo.


Hivyo, miongoni mwa makundi yalio hatarini zaidi ni watoto ambao kawaida hutembea na kucheza bila viatu, na pia hupendelea kula udongo. Pia baadhi ya wanawake waja wazito wana tabia ya kula udongo.

Athari za ugonjwa huu, iwapo hautatibiwa mapema, ni pamoja na kupungukiwa damu mwilini, matatizo ya moyo, kudumaa kimwili na kiakili.

Njia ya uhakika ya kuthibitisha iwapo mtu ameambukizwa minyoo ya safura ni kwenda kituo cha afya au hospitali na kupimwa choo katika maabara.

Homa ya matumbo (taifodi)

Homa ya matumbo ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea aina ya salmonella ambavyo huenezwa kupitia kinyesi na kuingia kwenye mwili wa binadamu kwa njia ya mdomo. Vimelea hivyo humwingia mtu kwa kunywa maji au kula chakula ambacho kimechafuliwa na kinyesi chenye vimelea hivyo.

Dalili za homa ya matumbo ni pamoja na: kukosa hamu ya kula; maumivu ya kichwa; maumivu mbalimbali; homa; na kuhara. Homa ya matumbo hujitokeza kati ya wiki moja au mbili baada ya kuambukizwa.

Dalili za homa ya matumbo mara nyingi hufanana na dalili za malaria. Hivyo, njia ya uhakika ya kuthibitisha iwapo mtu ameambukizwa homa ya matumbo au hapana ni kipimo cha maabara hospitalini au kwenye kituo cha afya.

Kuhara damu

Ugonjwa wa kuhara damu unaweza kusababishwa na ambukizo la amiba au wakati mwingine bakteria iitwayo shigella ambazo huathiri matumbo ya mwanadamu na kusababisha madhara mbalimbali yakiwemo vidonda kwenye matumbo, maumivu wakati wa kujisaidia, mharo wenye mchanganyiko wa damu na kamasi, na maumivu ya tumbo. Wakati mwingine, uambukizo wa amiba huambatana na homa kali na huweza kusababisha kufunga tumbo.

Maambukizi ya vimelea vya amiba hupitia kwenye maji au chakula kilichotayarishwa katika mazingira machafu. Mazingira hayo machafu hurahisisha chakula, maji na vyombo vyake kuchafuliwa na vimelea hivyo na hatimaye kuingia katika mwili wa binadamu, hasa iwapo chakula hakitachemshwa vya kutosha, au vyombo kutakashwa.

Maambukizi ya bakteria inayosababisha ugonjwa wa kuhara damu pia yanaweza kuenea haraka kutoka kwa mtu moja mwenye ugonjwa huo hadi mwingine kupitia chakula, maji, kushirikiana taulo, vyoo vya kukaa nk.

Mtu mwenye ambukizo la amiba naye huweza kujisaidia kinyesi chenye mayai ya vijidudu hao. Hivyo anaweza kueneza maambukizi iwapo hatatibiwa, kutumia choo kwa usahihi na kuzingatia kanuni za afya kuhusiana na maji na chakula. Hivyo inashauriwa kila mwenye dalili za maambukizi ya amiba, hususan kuharisha kinyesi chenye mchanganyiko wa damu na kamasi kuwahi hospitali au kwenye kituo cha afya kutibiwa.

Ukurasa huu ulihuishwa: 04 Juni 2022