Hesperian Health Guides

Visima ambavyo vimehifadhiwa au kujenga

Katika sura hii:

Kuna aina kadhaa za visima kwa ajili ya uvunaji wa maji yaliyo chini ya ardhi. Kisima rahisi zaidi ni kile kinachochimbwa kwa kutumia mikono na vifaa vya kawaida kama vile jembe na sururu. Lakini vipo visima vifupi vyenye kina hadi futi 18. Kisima kirefu chenye gharama kubwa kinaweza kuwa na kina cha zaidi ya futi 60. Visima vya aina hii kawaida hufungwa pampu iliyounganishwa na bomba kwa ajili ya kuvuta maji.

Kimsingi kisima kinachofaa ni kile ambacho kinaweza kuzalisha maji safi na salama na watu wakaweza kupata maji hayo. Ujenzi wa kisima bora, kwa jamii yoyote ile, hutegemea umbali yalipo maji chini ya ardhi na rasilimali zilizopo kwa ajili ya uchimbaji, kutoboa miamba na kukijengea pia.

Mara nyingi, visima vifupi vya kawaida, ambapo watu huchota maji kwa kutumia ndoo, vinaweza kuwa bora zaidi kuliko visima vya gharama kubwa ambavyo huhitaji pampu ili kuvuta maji. Vilevile visima vifupi kadhaa mara nyingi ni bora kuliko kisima kirefu kimoja, kwa sababu iwapo kisima kimoja kitakauka au kuharibika vingine vinaweza kuendelea kutoa huduma ya maji.

Hatua muhimu katika kuimarisha usalama wa visima

Kabla ya kuchimba kisima, jiulize: je aina hiyo ya kisima inayotarajiwa kujengwa ndiyo inafaa mahitaji ya kila mmoja? Maji yanaweza kuchafuliwa iwapo kisima kitachimbwa:

  • Karibu sana na choo cha shimo, mabomba ya maji taka, mashimo ya taka, au eneo la kuhifadhia, kuchungia mifugo. Angalau, kisima kiwe umbali wa mita 30.
  • Karibu na shughuli za viwanda kama vile uchimbaji madini, mafuta, mahali ambapo viuatilifu au mbolea za kemikali hutumika, au kwenye dampo za taka, na
  • Mahali ambapo maji taka au maji machafu yanaweza kutiririka na kuingia kwenye kisima.

Visima vifupi vilivyochimbwa kwa mkono vinaweza kutoa maji mazuri na salama. Lakini visima hivi vinaweza kukauka au kuchafuliwa kwa urahisi. Nyakati za mvua, maji yanayotiririka juu ya ardhi yanaweza kuingia katika visima hivyo, yakiwa yamebeba vijidudu vya magonjwa na uchafu mwingine. Watu au wanyama wanaotumia maji wanaweza kubeba vijidudu vya magonjwa kwenye miguu yao na kuviingiza kisimani. Ndoo na kamba zinazotumika kuchotea maji zinaweza pia kukusanya vijidudu, na kuchafua maji kwa urahisi pale zinapoingizwa kisimani. Uchafuzi wa visima hivyo unaweza kupungua kwa kuchukua hatua rahisi kadhaa. Kwa mfano:

  • Hakikisha kwamba ndoo na kamba zilizo safi tu ndizo zinazoingizwa kwenye maji.
  • Kisima kijengewe jukwaa la matofali au zege kulinda usalama wa maji kisimani.
  • Jenga kuta za kisima ili kupunguza hatari ya maji kukauka au kisima kubomoka, na pia.
  • Refusha kina: kina kirefu huweza kuhifadhi maji mengi zaidi.


Kabla ya kuchimba visima vipya au kufanya maboresho ya miradi ya maji yenye gharama kubwa, fikiria kwanza maboresho madogo madogo, kutegemea aina ya kisima, ili kuinua usalama wa chanzo hicho.

Maboresho katika visima vya kawaida na vya asili

EHB Ch6 Page 78-1.png EHB Ch6 Page 78-2.png
1. Kisima cha asili ambacho hakijaboreshwa 2. Mdomo wa kisima cha asili umejengwa sakafu yenye umbo la tuta ili kuzuia maji yanayotiririka yasiingie ndani
EHB Ch6 Page 78-3.png EHB Ch6 Page 78-4.png
3. Mdomo wa kisima cha asili umefunikwa kwa pipa 4. Mdomo wa kisima umeimarishwa kwa kujengewa kwa matofali na mwinuko wa kuondoa maji
EHB Ch6 Page 78-5.png EHB Ch6 Page 78-6.png
5. Kisima cha asili kimehifadhiwa na {{#drainage|kujengewa mfereji wa kuondoa maji]] 6. Kisima kilicho hifadhiwa, kimejengewa mfereji wa kuondoa maji, na bustani ndogo kutengenezwa ili kutumia ipasavyo maji yanayotiririka

Hifadhi kisima cha familia

Jamii nyingi zina visima virefu vinavyotumia pampu kuvuta maji ambavyo vimejengwa na serikali, mashirika yasio ya kiserikali ya ndani au ya kimataifa. Visima hivi virefu ambavyo vimefunikwa hulinda maji ili yasichafuliwe na watu au wanyama. Lakini miaka kadhaa baada ya kuchimbwa, visima vingi havitumiki kwa sababu pampu zake zimeharibika, au vipuri vyake havipatikani tena. Au watu wenye ujuzi wa kufanyia pampu hizo matengenezo hawapo tena. Hali hii husababisha uhaba wa maji safi. Watu hulazimika kutembea umbali mrefu kutafuta na kuchota maji yasiyo salama ili kukidhi mahitaji yao. Katika baadhi ya sehemu za bara la Afrika, visima vya familia vilivyojengewa vimeanza kuchukua nafasi ya visima virefu.

Kisima kilichojengewa ni shimo lililochimbwa kwa mkono na kuta zake kujengewa kwa matofali, kuwekewa mfuniko wa zege, mfumo wa kupandisha maji kawaida unaotumia kamba, na sakafu ya kukusanya na kuondoa maji yanayomwagika wakati wa kuchota. Kila hatua ya maboresho huongeza usalama wa kisima. Hatua hizi, pamoja na utunzaji makini wa maji, hufanya kisima cha familia kuwa salama zaidi.

Kisima kichimbwe wapi?

2 men digging a well.

Katika kutafuta sehemu ya kuchimba kisima, ishara muhimu kwamba huenda mahali hapo kuna maji ardhini ni kuwepo visima vingine karibu. Lakini iwapo visima vilivyopo karibu ni virefu, maji yanaweza kuwa chini sana na siyo rahisi kupatikana kwa kuchimba kwa mkono.

Ishara nyingine muhimu ni kuwepo uoto unaopendelea sana maji mengi. Maeneo ya bondeni kawaida yana uwezekano mkubwa wa kuwa na maji kuliko kwenye miinuko. Lakini iwapo kisima kitachimbwa bondeni, kitahitaji kulindwa dhidi ya mtiririko wa maji ya mvua kutoka kwenye miinuko.

MUHIMU! Kamwe usinywe maji moja kwa moja kutoka kisimani. Maji kutoka kisimani yanafaa kuchemshwa na kuchujwa kwa kutumia kitambaa safi kabla ya kuyanywa. Hii husaidia kuua na kuondoa baadhi ya uchafu.

Kuta za kisima

Katika udongo mgumu sana, huenda kusiwe na haja ya kujengea kisima ili kuzuia kisibomoke. Hata hivyo, ni muhimu kujenga angalau mita 1 hadi 2 chini ya ardhi ili kuzuia kuta za kisima kubomoka. Iwapo kisima chote kitajengwa kitakuwa imara zaidi. Hata hivyo, baadae, uchimbaji kwa ajili ya kurefusha kina utakuwa mgumu. Kisima kinaweza kujengwa kwa kutumia mawe au miamba, matofali ya mchanga, matofali ya kuchoma au zege.

EHB Ch6 Page 79-2.png
EHB Ch6 Page 79-3.png
Mita 1 hadi 2 za juu zimejengwa Kisima chote kimejengewa
Jinsi ya kutengeneza mfuniko wa kisima

Mara baada ya kisima kujengewa, hatua inayofuata ni kuweka mfuniko wa zege. Mfuniko unasaidia kuzuia maji machafu au vitu mbalimbali kupenya kisimani. Pia huchangia kisima kuwa salama zaidi kwa watoto na kuwepo sehemu safi ya kuweka ndoo pale watu wanapokuwa wanachota maji.

EHB Ch6 Page 80-1.png
Tengeneza umbo la mfuniko.
EHB Ch6 Page 80-2.png
Weka utando wa nondo na umbo la mdomo wa kisima.
EHB Ch6 Page 80-3.png
Mwaga zege kutengeneza kingo za mdomo wa kisima.
EHB Ch6 Page 80-4.png
Tengeneza vizuri kingo za mdomo wa kisima.
EHB Ch6 Page 80-5.png
Weka mfuniko wa kisima mahali pake.
  1. Mfuniko unapaswa kufunika vizuri mlango wa kisima. Safisha eneo tambarare kwa ajili ya kumwanga zege. Chora umbo la mduara wenye vipimo vinavyolingana na mlango wa kisima. Weka mzunguko wa matofali kuzunguka mduara uliochorwa. Mduara huo ndiyo utajazwa tabaka la zege kwa ajili ya kutengeneza mfuniko.
  2. Acha nafasi katikati inayotosheleza ndoo kupita au kufungia pampu. Ukubwa wa nafasi hiyo utategemea aina ya ndoo au pampu itakayotumika. Kwa ujumla, nafasi hii inafaa kutosheleza kupitisha ndoo ya lita 10.
  3. Weka nondo za milimita 3 ili kuimarisha mfuniko, sentimeta 10 kutoka nondo moja hadi nyingine, na kuzifuma pamoja ili kutengeneza utando.
  4. Ondoa utando wa nondo na changanya zege kwa kutumia vipimo vitatu vya kokoto, vipimo viwili vya mchanga na kipimo kimoja cha saruji. Iwapo huna kokoto, tumia vipimo vinne vya mchanga na kimoja cha saruji. Mwaga zege hadi nusu ya kina cha mduara ulioandaliwa kwa ajili ya kutengenezea mfuniko. Weka utando wa nondo uliotengenezwa juu ya zege ambayo haijakauka. Mwaga zege iliyobaki kujaza na kusawazisha mduara kwa kutumia kipande cha ubao.
  5. Acha mfuniko huo kuimarika kwa muda wa saa 1. Ondoa ndoo iliyowekwa katikati kwenye nafasi ya kuchotea maji au kufunga pampu. Jaza nafasi hiyo kwa mchanga ulioloweshwa maji. Weka tena ndoo juu ya mchanga, na panga matofali kuzunguka ndoo hiyo, ukiacha milimita 75 kati ya pipa na matofali. Jaza nafasi kati ya pipa na matofali kwa kutumia zege na kuacha iimarike kwa muda wa saa 1. Baada ya saa 1 ondoa matofali na pipa kisha tengeneza vizuri kingo za mlango wa kisima.
  6. Acha mfuniko huo ukauke usiku huo na kuendelea kuumwagilia maji angalau kwa siku tatu ili uweze kuimarika vyakutosha. Baada ya siku 7, pima uimara wa mfuniko huo kwa kuweka vipande 4 vya mbao ili kuuinua kutoka ardhini. Halafu simama juu yake. Mfuniko wa kisima ambao umetengenezwa vizuri hautavunjika hata watu kadhaa wakirukaruka juu yake. Weka ukingo wa saruji kuzunguka eneo la juu la ukuta wa kisima na, kwa uangalifu sana, weka mfuniko wa kisima mahali pake.


Uchotaji maji kutoka kisimani kwa kutumia gongo lenye roda, ndoo na kamba au myorororo

Gongo lenye roda ni mti au chuma kilichofungwa mkono wa kuzungusha ambacho hurahisisha ndoo kupandishwa kutoka kisimani na pia kutoa nafasi ya kuzungushia mnyororo au kamba. Iwapo pampu itafungwa kwenye kisima hapo baadaye, gongo lenye roda linaweza kuondolewa kwa urahisi. Funga ndoo mwishoni mwa mnyororo au kamba. Mnyororo ni bora kwa sababu ni vimelea vichache ambavyo vinaweza kuzaliana kwenye mnyororo. Hata hivyo, mnyororo ni ghali kuliko kamba. Kamba haina gharama kubwa na inaweza kuwekwa nyingine iwapo itakatika.

EHB Ch6 Page 81-1.png
Jengea nguzo ya kubeba gongo lenye roda katika kila upande.
Tengeneza meno kwenye nguzo kwa ajili ya kubeba gongo.
EHB Ch6 Page 81-2.png
Funga misumari ya boliti juu ya gongo ili gongo libaki kwenye nafasi yake linapozunguka.
Michoro hii inaonyesha nguzo za mti kwa ajili ya gongo lenye roda zikisimikwa ardhini. Nguzo hizi pia zinaweza kujengwa kwa matofali.

Jukwaa na mfereji wa kuondoa maji

Jukwaa na mfereji wa kuondoa maji yanayomwagika kutoka kisimani wakati wa uchotaji husaidia kulinda usafi wa kisima. Mfereji huu huepusha eneo linalozunguka kisima kuwa na matope, hali ambayo ingeweza kusababisha mazalia ya vimelea vya magonjwa na wadudu. Vimelea vinaweza kuzaliana kwenye nyufa na mashimo. Hivyo ni muhimu jukwa na mtaro wake kujengwa vizuri.

EHB Ch6 Page 81-3.png
Mnyororo au kamba ya ndoo hubaki ikiwa imeviringishwa kwenye gongo la roda.
Gongo lenye roda
Ndoo huning’inizwa kwenye mkono wa gongo lenye roda ili kutunza usafi
Mfuniko wa kisima
Mfereji wa mita 2-3 pale inapowezekana
Jukwa lenye upana wa mita 2
Mwaga zege yenye kina cha milimita 75, na milimita 150 za ukingo kuzunguka eneo hilo. Jukwa zima na ukingo wake viimarishwe kwa nondo za milimita 3 ili kuzuia nyufa.

Tunzeni vizuri kisima chenu

Maji kisimani yanaweza kuchafuliwa kwa urahisi pale ndoo chafu na kamba au minyororo michafu vikitumbukizwa ndani yake. Ili kulinda usalama wa maji kisimani, tenga ndoo moja maalum kwa ajili ya kuchotea ambayo itakuwa imefungwa kwenye kisima wakati wote. Ndoo hiyo tu ndiyo itumike kujazia vyombo vingine. Ni muhimu kunawa mikono kabla ya kuchota maji na kujenga uzio kuzunguka kisima hicho ili kuzuia wanyama na uchafuzi wa maji.

EHB Ch6 Page 82-1.png

Bomba la jamii lenye mfereji wa kuondoa maji yaliyomwagika
EHB Ch6 Page 82-arrow.png
EHB Ch6 Page 82-2.png
Shimo kwa ajili ya kunyonya maji
Mawe makubwa
Kokoto
Mchanga

Mnaweza pia kulinda usalama wa maji ya kisima chenu kwa:

  • Kuhakikisha mfuniko wa kisima umekaa ipasavyo.
  • Kuhakikisha usafi wa jukwaa na mfereji wa kuondoa maji yanayomwagika wakati wa kuchota au kuosha vyombo vya kuchotea.
  • Kulainisha mashine ya kuzungushia kamba na mafuta ya girisi mara kwa mara ili iweze kutumika kwa urahisi.
  • Kutoruhusu watoto kuchezea kisima au pampu.
  • Kujenga uzio kuzunguka kisima ili kuzuia mifugo.
  • Kuweka mtu maalum wa kusimamia kisima.

Weka mfumo wa kuondoa maji yanayomwagika kutoka kisimani au kwenye bomba za maji wakati wa uchotaji

Kila wakati watu wanapochota maji kisimani, kiasi fulani cha maji humwagika. Maji hayo yakijikusanya, yanaweza kutengeneza vidimbwi na kugeuka kuwa mazalia ya mbu ambao husambaza malaria na magonjwa mengine. Visima, mabomba, matoleo kwenye tenki za maji na sehemu nyingine za kuhifadhi maji huhitaji mifereji ya kuondoa maji yanayomwagika ili yaweze kuondolewa vizuri, kunyonywa na ardhi, au kutumika kwa ajili ya bustani ndogo.

Ili maji yanayomwagika yaweze kutumika vizuri, panda mti au bustani ya mboga eneo maji yanapotiririkia. Kama huwezi kupanda mti au bustani, chimba shimo la kupokea maji hayo, lijazwe mchanga, kokoto na mawe. Shimo hili la kunyonya maji yanayotirika husaidia kuzuia mbu kuzaliana.

Kutumia pampu kupandisha maji kutoka kwenye kisima

Ili kupandisha maji juu kutoka kisimani, pampu inatakiwa. Pampu hutumia aina mbalimbali za nishati, ukiwemo umeme, gesi, nishati ya jua au nguvu ya binadamu. Iwapo pampu haiwezi kutumika kwa urahisi au haifanyi kazi, watu kawaida huanza kuchota maji kutoka vyanzo visivyo salama.

Namna ya kuchagua pampu inayofaa

Pampu za aina nyingi hufanana kwa kitu kimoja: zikiharibika maji hayawezi kupatikana. Kwa watu wengi, pampu bora ni ile ambayo wanaweza kutengeneza, kutumia kwa urahisi na kuifanyia matengenezo wenyewe pale inapoharibika, au kutumia mafundi wanaoaminika waliopo katika jamii yao. Hivyo, ni muhimu kufikiria mambo yafuatayo wakati wa kuchagua pampu:

  • Je itaweza kutumiwa kwa urahisi na wote - wanawake na wanaume na kukidhi mahitaji yao? Je, wanawake walishirikishwa katika kuichagua pampu inayofaa?
  • Je kuna aina gani ya nishati katika jamii husika? Iwapo jamii itachagua aina ya pampu inayotumia mafuta yenye gharama kubwa, au umeme ambao haupo, haitakuwa na manufaa.
  • Je pampu hiyo inaweza kufanyiwa matengenezo kwa urahisi na vipuri vyake vinapatikana? Je, ni vyema kuwa na pampu isiyo imara sana lakini inatengenezeka kwa urahisi na wanajamii, au pampu ambayo ni imara lakini pale inapoharibika haiwezi kutengenezwa kwa urahisi na mafundi waliopo katika jamii?

Pampu ya kamba: teknolojia rahisi na yenye gharama nafuu ya kupandisha maji kutoka kisimani

EHB Ch6 Page 83-1.png

Pampu ya kamba hutengenezwa kutokana na vifaa imara vyenye gharama nafuu.
Ringi la baiskeli au gongo lenye roda na mkono wake
Usawa wa ardhi
Usawa wa maji
Kamba
(isikaze sana)
Diski za mpira
Bomba la nchi 1½ au sentimeta 4
Vibanio vya mpira
Bomba la nchi 1½ au sentimeta 4
Kiunganishi cha bomba nchi 1½ au sentimeta 4
Ndoo

Pampu ya kamba msingi wake ni usanifu uliotumiwa zamani huko China. Pampu hii hutumika kupandisha maji kutoka kwenye visima hadi mita 15 kwa kutumia nguvu kidogo. Kadri mtu anapozungusha gurudumu, maji hupanda na kumwagika kupitia bomba lililopo juu ya kisima.

Pampu hii huhitaji gharama kidogo kutengeneza na ni rahisi kufunga. Ndiyo, kamba mara nyingi hukatika, lakini ni rahisi kufunga nyingine au kuunganisha kamba iliyokatika, na baada ya hapo pampu ikaendelea kufanya kazi. Watu katika nchi nyingi wameamua kuchagua teknolojia ya pampu ya kamba kulingana na mahitaji yao na na rasilimali walizo nazo.


Ukurasa huu ulihuishwa: 04 Juni 2022