Hesperian Health Guides

Dawa za kutibu sumu

Huduma ya kwanza: Madawa

Dawa ya mkaa ya kunyonya sumu mwilini (activated charcoal)


Dawa ya mkaa ya kunyonya sumu mwilini ni mkaa ambao umetengenezwa katika utaratibu maalum na kuamilishwa kwa ajili kutibu madhara ya sumu yanayosababishwa na vitu mbalimbali kama vile kumeza baadhi ya dawa za viuawadudu na viua magugu. Dawa ya mkaa huzuia sumu isinyonywe na mwili. Hivyo toa dawa hii kwa mgonjwa haraka mara baada ya tukio la kula au kunywa sumu. Dawa ya mkaa ya kunyonya sumu mwilini haina madhara. Mpe mtu ambaye unadhani amelishwa sumu, hata kama huna uhakika.

Kama huna dawa hii ya mkaa, unaweza kutumia unga wa mkaa wa kawaida kutokana na kuni au miti iliyochomwa. Chaganya kijiko 1 cha unga wa mkaa na maji yenye vuguvugu kwenye glasi kubwa. Unga huu siyo mzuri kama dawa ya mkaa ambayo imeongezewa uwezo, lakini unakidhi.

Kamwe usitumie unga wa mkaa ambao umetengenezwa kutokana na taka (charcoal briquettes)— ni sumu!

Hata hivyo, dawa ya mkaa ya kunyonya sumu haisaidii dhidi ya sumu ambazo zinatokana na:

  • vibabuzi kama vile ammonia, betri, asidi, dawa ya kusafisha mitaro, soda magadi kali
  • haidrokaboni kama vile mafuta ya gari au mitambo, mafuta ya taa, dawa za kusafisha na kuyeyusha rangi, kaboliki asidi, kafuri (camphor) nk
  • sinaidi ambayo hutumika kwenye shughuli za madini, viwandani, usindikaji wa ngozi za wanyama, sumu ya panya
  • ethano (ethanol)
  • chuma - vidonge vya chuma, vitaminimseto au vitamini inayotolewa mtoto angali tumboni (prenatal vitamins).
  • lithiamu (lithium) - hupatikana katika baadhi ya dawa za kutibu matatizo yanayohusiana na ugonjwa wa akili.
  • methano (methanol) hupatikana kwenye dawa ya kusafisha sakafu, dawa za kulainisha rangi, kemikali zinazoongezwa kwenye mafuta ya gari
  • asidi zinazotokana na madini
  • viyeyushaji vyenye asili ya kaboni (organic solvents) ambavyo hupatikana kwenye dawa za kulainisha rangi,dawa za kusafisha gundi, kemikali za kusafisha rangi ya kucha, dawa za kusafisha madoa
Madhara ya pembeniGreen-effects-nwtnd.png

Huweza kusababisha kinyesi cheusi, kutapika, choo kigumu au kukosa choo kwa muda mrefu, au kuharisha.

Jinsi ya kutumia

Toa mara baada ya tukio la sumu (au uwezekano wa usumishaji) na glasi iliyojaa maji. Dozi inaweza kutolewa tena ndani ya saa 4.
Chini ya mwaka 1: mpe gramu 10 hadi 25.
Mwaka 1 hadi 12: mpe gramu 25 hadi 50.
Zaidi ya miaka 12: mpe gramu 50.

Atropini (atropine)


Atropini hutumika kutibu usumishaji kutokana na viuadudu waharibifu, viuadudu wa nyumbani, au gesi ambazo hudhofisha mfumo wa neva. Tumia Atropini tu kama jinsi karatasi ya maelekezo juu ya kiuadudu hicho inavyoelekeza. Kiasi cha atropini ambacho kinahitajika hutegemea ukali wa tukio la sumu. Kawaida, sumu kutokana na kabameti (carbamate) huhitaji dawa kidogo kuliko sumu kutokana na oganofosfeti (organophosphate).

Madhara ya pembeniGreen-effects-nwtnd.png

Kusinziasinzia, kupepesuka, maumivu ya kichwa, mabadiliko katika kufikiri, na kinyesi kigumu.

MuhimuNBgrnimportant.png

Mweke mgonjwa sehemu yenye ubaridi baada ya kumpa atropini.

Jinsi ya kutumiaNBgrninject.png
Choma kwenye msuli.
Chini ya miaka 2: choma miligramu 0.05 kwa kilo, kila dakika 5 hadi 10.
Miaka 2 hadi 10: choma miligramu 1, kila dakika 5 hadi 10.
Zaidi ya miaka 10: choma miligramu 2, kila dakika 5 hadi 10.

Usitoe sindano ya atropini kama utaona ngozi inavimba na kukaukia, na mboni za jicho kuongezeka ukubwa. Kama tukio la sumu ni kali, zidisha mara mbili kiasi cha atropini kilichoelezwa hapo juu.

Deferoksamini (deferoxamine)


Deferoksamini husaidia kutibu matukio ya sumu kutokana na madini chuma yenye sumu kwa kuyaondoa kwenye damu.

Madhara ya pembeniGreen-effects-nwtnd.png

Uoni hafifu na mabadiliko katika kufikiri.

MuhimuNBgrnimportant.png

Usitoe kwa mgonjwa wa figo au kama hawezi kukojoa.Usitoe kwa watoto chini ya miaka 3.

Jinsi ya kutumiaNBgrninject.png
Choma polepole kwenye msuli. Choma miligramu 50 kwa kilo, kila saa 6.Usitoe zaidi ya gramu 6 kwa siku. Kama huwezi kumpima mtu, toa dozi kwa kuzingatia umri:
Chini ya miaka 5: polepole choma miligramu 550, kila saa 6, kwa siku 1 (mara 4).
Miaka 5 hadi 12: polepole choma miligramu 1000, kila saa 6, kwa siku 1 (mara 4).
Zaidi ya miaka 12: polepole choma kila saa 6 kwa siku 1: miligramu 2000 (mara 2), baada ya hapo miligramu 1000 (mara 2).

Asetisisteni (acetylcysteine)


Toa asetisisteni haraka iwezekanavyo baada ya kutumia asetaminofeni (acetaminophen) iliyozidi kipimo kinachohitajika. Asetaminofeni iliyozidi kipimo kinachohitajika ni zaidi ya miligramu 7,000 kwa mtu mzima, na zaidi ya miligramu 140 kwa kilo kwa mtoto.

Asetisisteni ina harufu kali. Kuichanganya na juisi husaidia mgonjwa kuivumilia.

Jinsi ya kutumiaNBgrnspoon.png

Kwa ajili ya asetaminofeni (parasetamo) iliyozidi kiasi kinachohitajika

Toa miligramu 140 kwa kilo kwa njia ya mdomo. Subiri hadi saa 4 halafu mpe miligramu 70 kwa kilo kwa njia ya mdomo,na kuendelea na kiasi hiki kila saa 4, mara 17. Kama mtu atatapika ndani ya saa 1 ya kutumia dawa hii, mpe dozi hiyo tena.

Naloksoni (naloxone)


Naloksoni hutumika kutibu madhara ya kuzidisha kiasi cha dawa za kupunguza mauvimu kutoka kundi la dawa kali za kupunguza maumivu zenye asili ya afyuni (opioids). Dawa hizo ni kama vile mofini (morphine), heroini, methadoni (methadone), afyuni (opiamu), oksikodoni (oxycodone), na madawa mengine kali ya kupunguza maumivu.Toa naloksoni hadi mtu atakapoweza kupumua vizuri mwenyewe. Nguvu ya dawa mwilini inaweza kupungua baada ya muda. Hivyo toa dozi nyingine baada ya dakika 20 kama ataanza kupumua kwa shida tena.

Madhara ya pembeniGreen-effects-nwtnd.png

Kichefuchefu, kutapika, na kutokwa na jasho. Kukosa raha kabisa.

Jinsi ya kutumiaNBgrninject.png
Chini ya miaka 5 au mtoto mwenye uzito chini ya kilo 20: choma miligramu 0.1 kwa kilo katika msuli kila dakika 2 hadi 3 kadri itakavyohitajika, lakini usitoe zaidi ya miligramu 2 kwa ujumla.
Zaidi ya miaka 5 au mtoto mwenye uzito zaidi ya kilo 20: choma ½ miligramu hadi miligramu 2 kwenye msuli. Kama itahitajika, rudia dozi kila dakika 2 hadi 3, lakini usitoe zaidi ya miligramu 10 kwa ujumla.

Sodiamu naitraiti (sodium nitrite)


Sodiamu naitraiti hutumika kutibu matukio ya sumu kutokana sinaidi pamoja na sodiamu thiosalfeti (sodium thiosulfate). Lazima ichomwe kwenye mshipa. Usichome sindano hii kama hujui jinsi ya kuichoma.

Jinsi ya kutumiaNBgrninject.png
Choma sindano ya sodiamu naitraiti polepole kwa dakika 5 hadi 20 kwenye mshipa.
Chini ya miaka 12: choma miligramu 4 hadi 10 kwa kilo kwenye mshipa. Usitoe zaidi ya miligramu 300
Zaidi ya miaka 12: choma miligramu 300 kwenye mshipa.

Fuatisha sindano ya sodiamu thiosalfeti. Angalia chini kwa ajili ya dozi.

Sodiamu thiosalfeti (sodium thiosulfate)


Sodiamu thiosalfeti hutumika kutibu tukio la sumu kutokana na sinaidi, pamoja na sindano ya sodiamu naitraiti. Lazima ichomwe kwenye mshipa. Usichome sindano hii kama hujui jinsi ya kuichoma.

Jinsi ya kutumiaNBgrninject.png
Choma sindano ya sodiamu thiosalfeti polepole kwa muda wa dakika 10 kwenye mshipa.
Chini ya miaka 12: choma miligramu 400 kwa kilo kwenye mshipa.
Zaidi ya miaka 12: choma gramu 12.5 kwenye mshipa.