Hesperian Health Guides

Vitamini na viongeza madini mwilini (mineral supplements)

Kuwatunza watoto: Madawa

Vitamini A, retino (retinol)


Kuzuia uoni hafifu wa usiku na zerofthalmia

Katika maeneo ambapo matatizo ya uoni hafifu usiku na zerofthalmia (kukauka na kuongezeka ukubwa wa konea) yameenea sana, watu wanahitaji zaidi matunda ya njano na mbogamboga za kijani, pamoja na vyakula kutokana na wanyama kama vile mayai na maini. Kwa kuwa vyakula hivyo mara nyingi havipatikani – angalau kwa muda mfupi–ni bora kuwapatia watoto na mama zao matone ya vitamini A mwilini kila baada ya miezi 6.

MuhimuNBgrnimportant.png

Kawaida huwezi kupata Vitamini A inayozidi kiwango ambacho mwili unahitaji kutoka kwenye chakula. Lakini kuzidisha vidonge vya vitamini au mafuta ni hatari. Usitumie zaidi ya kiwango ambacho kimependekezwa.

Jinsi ya kutumiaNBgrnpill.png

Kwa watoto wadogo, unaweza kusaga vidonge na kuchanganya unga na maziwa kidogo ya mama. Au kata kidonge aina ya kapsuli na kukamulia majimaji yaliyomo mdomoni mwa mtoto.

Kuzuia upungufu wa vitamin A mwilini
Miezi 6 hadi mwaka 1: toa uniti 100,000 kwa njia ya mdomo mara moja.
Zaidi ya mwaka 1: toa uniti 200,000 kwa mdomo mara moja. Rudia baada ya miezi 6.
Kwa akina mama: toa uniti 200,000 kwa mdomo ndani ya wiki 6 baada ya kujifungua. Vitamini A itamkinga mama na pia kumfikia mtoto kupitia maziwa ya mama.
Kwa watoto wenye surua
Vitamini A huzuia nimonia na upofu, matatizo 2 ya kawaida yanayohusiana na surua.
Miezi 6 hadi mwaka 1: toa uniti 100,000 kwa njia ya mdomo, mara 1 kila siku kwa siku 2.

Zaidi ya mwaka 1: toa uniti 200,000 kwa njia ya mdomo, mara 1 kila siku kwa siku 2. (Kama mtoto alipata dozi ya vitamini A katika miezi 6 iliyopita, mpe dozi hii kwa siku 1 tu.)

Iwapo mlengwa ana hali mbaya sana ya lishe au tayari ameanza kupoteza uwezo wake wa kuona, rudia dozi ya vitamini A baada ya wiki 2.

Zinki (Zinc)


Madini ya zinki husaidia watoto wanaoharisha kupata nafuu haraka. Madini hayo yanapaswa kutolewa pamoja na kinywaji cha kuongeza maji mwilini.

Jinsi ya kutumiaNBgrnpill.png
Kwa watoto, vidonge vinaweza kusagwa na kuchanganywa na maziwa ya mama au na maji kidogo. Pia unaweza kupata aina ya kidonge ambacho humomonyoka haraka na kuchanganyika kwa urahisi kwenye kimiminika.
Watoto wachanga hadi miezi 6: toa miligramu 10, mara 1 kila siku kwa siku 10 hadi 14.
Zaidi ya miezi 6: toa miligramu 20, mara 1 kila siku kwa siku 10 hadi 14.

Madini ya chuma, ferasi salfeti, ferasi glukoneti (iron, ferrous sulfate, ferrous gluconate)


Vyongeza madini ya chuma husaidia katika kutibu au kuzuia matukio mengi ya upungufu wa wekundu wa damu mwilini. Matibabu kwa kutumia vyongeza madini ya chuma kawaida huchukua angalau miezi 3.

Vyongeza madini ya chuma hufanya kazi vizuri vinapotumiwa pamoja na vitamini C (aidha kwa kula matunda na mbogamboga, au kutumia kidonge cha vitamini C).

Madhara ya pembeniGreen-effects-nwtnd.png

Vyongeza madini ya chuma wakati mwingine huvuruga tumbo na ni bora kutumiwa na chakula. Vilevile, vinaweza kusababisha shida katika kupata choo hasa kwa watu wazima, na kufanya kinyesi kuonekana cheusi.

Kunywa viongeza madini ya chuma vinavyomiminika huyafanya meno kuonekana meusi. Kunywa kwa kutumia mrija au piga meno mswaki baada yakunywa.

MuhimuNBgrnimportant.png

Hakikisha dozi ni sahihi. Ukizidisha hugeuka sumu. Usitoe viongeza madini ya chuma kwa watu walioathirika sana kilishe. Subiri hadi afya zao zirudi ndipo uwape madini ya chuma.

Jinsi ya kutumiaNBgrnpillspoon.png

Miundo tofauti ya viongeza madini ya chuma huwa na ujazo tofauti wa madini hayo. Kwa mfano, kidonge cha ferasi salfeti chenye miligramu 300 huwa na miligramu 60 za madini ya chuma. Lakini kidonge cha ferasi glukoneti chenye miligramu 325 huwa na miligramu 36 za madini ya chuma. Hivyo, soma maelekezo kwenye kifungashio cha vidonge vyako, chupa ya dawa (au karatasi ya taarifa juu ya dawa), au taarifa juu ya viongeza madini ya chuma vingine kujua kiwango cha madini ya chuma kilichomo.

KUZUIA upungufu wa wekundu wa damu (anemia) miongoni mwa akina mama wajawazito na wanaonyonyesha
Toa ferasi salfeti miligramu 300 (miligramu 60 za madini ya chuma ) kila siku. Inapaswa kutumiwa kila siku na wanawake ambao wanapanga kupata mimba. Kuunganisha viongeza madini ya chuma na viongeza asidi ya foliki (folic acid) ni bora zaidi kwa sababu asidi ya foliki husaidia kuzuia hililafu katika uzazi.
KUTIBU mtoto mwenye upungufu wa wekundu wa damu (anemia)
Toa ferasi salfeti mara 1 kwa siku, au gawa katika dozi 2 iwapo itavuruga tumbo.
DOZI YA FERASI SALFETI KWA UMRI
KUNDI LA UMRI KIASI GANI KATIKA KILA DOZI VIDONGE VYA MILIGRAMU 300 VINGAPI JUMLA YA MADINI YA CHUMA
Chini ya miaka 2 Miligramu 125 za ferasi salfeti Tumia sairapu ya madini ya chuma, au saga ¼ kidonge cha ferasi salfeti chenye miligramu 300 kwenye maziwa ya mama Toa kiasi cha kutosha kutoa miligramu 25 za madini ya chuma
Miaka 2 hadi 12 Miligramu 300 za ferasi salfeti Kidonge 1 cha ferasi salfeti chenye miligramu 300 Toa kiasi cha kutosha kutoa miligramu 60 za madini ya chuma
Zaidi ya miaka 12 Miligramu 600 za ferasi salfeti Vidonge 2 vya ferasi salfeti vyenye miligramu 300 Toa kiasi cha kutosha kutoa miligramu 120 za madini ya chuma