Hesperian Health Guides

Mambo gani hufanya maji yasiwe salama?

Katika sura hii:

Maji yanakuwa siyo salama yanapokuwa na vijidudu vya magonjwa, minyoo au kemikali zenye sumu. Vijidudu vya magonjwa, viumbe vidogo sana ambavyo haviwezi kuonekana kwa macho, na minyoo, kama vile tegu na safura husababisha magonjwa mengi mabaya. Vijidudu hivi na minyoo huishi katika vinyesi vya binadamu na wanyama (mkojo na vinyesi) na huweza kusababisha magonjwa mabaya na ya muda mrefu pale ambapo:  A woman holds a pitcher of water while drinking from a glass.

  • Hakuna huduma nzuri ya vyoo na njia salama za kuondoa vinyesi vya wanyama.
  • Hakuna ulinzi na usafi wa kutosha wa vyanzo vya maji.
  • Hakuna maji ya kutosha kwa ajili ya kufanya usafi.


Baadhi ya magonjwa yanayohusiana na maji, kama vile kipindupindu, husambaa haraka na yanaweza kusababisha vifo vingi. Magonjwa mengine yanaweza kumfanya mtu kuugua kwa miaka mingi na kusababisha matatizo mengine ya kiafya kama vile kupungukiwa na maji mwilini, maambukizi mbalimbali, upungufu wa damu mwilini na utapiamlo. Kwa sababu dalili kuu ya magonjwa yanayosababishwa na vijidudu na minyoo mbalimbali ni kuharisha, magonjwa haya mara nyingi huitwa magonjwa ya kuhara.

Hadithi ya Timotheo

Njoki aliishi katika kijiji kimoja akiwa na mwanae wa mwaka mmoja Timotheo. Kama wanakijiji wengine alichota maji kutoka kwenye kisima kilichojengwa miaka mingi iliyopita na kikundi kimoja cha maendeleo. Huko nyuma pampu ilipoharibika, wanakikundi hao walileta vipuri vya kuikarabati. Lakini baada ya kikundi kicho kuhamia sehemu nyingine, hakuna hata mtu mmoja pale kijijini aliyejua namna ya kutengeneza pampu hiyo, wala sehemu ya kupata vipuri vyake. Pia hawakua na fedha za kununulia vipuri hivyo.


Kwa hiyo, pampu ilipoharibika, ilibidi wanawake kutembea umbali mrefu ili kuchota maji kwenye kisima cha asili nje ya kijiji hicho. Kisima hicho pia kilitumiwa na mifugo, na maji yake hayakuwa safi wala salama. Baada ya kunywa maji kutoka kwenye kisima hicho, Timotheo aliugua na kuanza kuharisha sana. Alianza kudhoofu haraka. Njoki hakuwa na fedha ya kumpeleka kwenye kituo cha afya, safari ambayo ilihitaji saa kadhaa. Baada ya siku chache, Timotheo alifariki.

Upungufu mkubwa wa maji mwilini kutokana na magonjwa ya kuhara ndio chanzo kikuu cha vifo vya watoto duniani. Mjadala wa namna watu wanavyoambukizwa magonjwa ya kuhara unaweza kuongozwa kwa kuuliza msururu wa maswali ya kwa nini?

Kufahamu kwa nini Timotheo alifariki

Zoezi la kuuliza maswali ya “Lakini kwa nini?” linaweza kusaidia katika kufahamu sababu mbalimbali za ugonjwa na kifo cha Timotheo.

Nini kilisababisha kifo cha Timotheo? Kuharisha na upungufu mkubwa wa maji mwilini.

Lakini kwa nini alipatwa na ugonjwa wa kuharisha? Kulikuwa na vijidudu vya ugonjwa huo kwenye maji aliyokunywa.

Lakini kwa nini kulikuwa na vijidudu vya ugonjwa huo kwenye maji? Kisima kilikuwa hakijajengewa na kuhifadhiwa, hivyo maji yake yalikuwa yamechafuliwa na vijidudu vya magonjwa pamoja na minyoo.

Lakini kwa nini Timotheo alikunywa maji ya kisima ambacho kilikuwa hakijajengewa na kutunzwa vizuri? Pampu ya kijiji ilikuwa imeharibika.

Lakini kwa nini haikuweza kutengenezwa?

A woman speaking.
Endeleza “mnyororo” hadi utakapoishiwa maswali. Unaweza pia kurejea majibu ya awali na kuulizia sababu za ndani zaidi. Kwa mfano:

Lakini kwa nini njoku hakuyatibu maji kabla ya kunywa? Kulikuwa na kuni kidogo kwa ajili ya kuchemsha maji na hakuna fedha kabisa kwa ajili ya kusafisha maji kwa kutumia klorini.

Maswali ya Lakini kwa nini? huendelea kadri watu watakavyokuwa wanatoa sababu mbalimbali za kifo cha Timotheo. Mnyororo wa sababu ukichorwa kwenye karatasi au ubao, unaweza kuonyesha jinsi gani kila sababu iliyotolewa inahusiana na sababu zingine. Kila sababu iliyotolewa huunganishwa kwenye mnyororo. Kwa njia hii watu wanaweza kuelewa sababu tofauti za magonjwa, na jinsi gani yanaweza kuzuiwa.

 chain links.

Pampu kuharibika
Vinyesi vya wanyama kwenye maji
Hakuna kuni za kuchemshia maji
Timotheo aambukizwa ugonjwa wa kuharisha
Hakuna kinywaji chenye mchanganyiko wa chumvi na sukari kwa ajili ya kuongeza maji mw
Hakuna fedha za kumlipa daktari
Timotheo afariki
Hadithi rahisi ya picha kuelezea jinsi vijidudu vya magonjwa vinavyoenezwa

 man defecating.
dog.
EHB Ch5 Page 48-5.png child with dog.
mother crouching near child.
1. Mtu anaharisha nje ya choo. 2. Mbwa anakula kinyesi cha mtu aliyeharisha. 3. Mtoto anacheza na mbwa na kujipaka kinyesi mikononi. 4. Mtoto anaanza kulia na mama yake anamtuliza. Mtoto anafuta mikono yake kwenye sketi ya mama.
 hand, cloth and griddle.
man, woman and two children.
 man, woman and two children looking ill.
5. Mama ananza kupika. Vijidudu vya ugonjwa kwenye sketi yake vinaingia mikononi mwake. Anapakua chakula kwa mikono yake. 6. Familia inakula chakula hicho. 7. Baadaye, familia nzima inaambukizwa ugonjwa wa kuhara.

Jinsi vijidudu vya magonjwa na minyoo vinavyosambaza maambukizi

Ni rahisi kujua mahali vilipo vijidudu vya magonjwa na minyoo - kwenye vitu vichafu kama vile vinyesi, vyakula ambavyo vimeoza, vyoo vichafu na vitu vingine. Lakini wakati mwingine vijidudu hivi vinaweza kupatikana sehemu ambazo zinadhaniwa kuwa safi, kama vile maji ambayo yanaonekana kwa macho kuwa safi, kwenye mikono yetu, vitasa vya milango, vidahizo vya kompyuta nk.

Vijidudu vya magonjwa na minyoo vinaweza kuenea kutoka mtu mmoja hadi mwingine kupitia kugusana, kwa njia ya hewa pamoja na vumbi, au watu wanapokohoa au kupiga chafya. Vinaweza kusambaa kupitia chakula na maji ya kunywa, au kubebwa na nzi, wadudu wengine na wanyama. Vinaweza pia kuishi kwenye vyakula ambavyo havijapikwa kabisa au kutopikwa vizuri. Baadhi ya minyoo inaweza kuenezwa kwa kunywa, kukanyaga, au kunawa maji machafu yenye minyoo hiyo, au kula mbogamboga na mimea mingine kutoka kwenye maji machafu. Vijidudu hao na minyoo ambao husababisha kuharisha husafiri kwa njia zifuatazo:

arrows showing path of germs from man defecating, to hand, flies, corn stalks and river, to cup and plate of food, to person eating.
Njia ambazo vijidudu vya magonjwa husafiria ni pamoja na: vidole, nzi, vinyesi, mashamba, vyakula na vitu vyenye asili ya majimaji (vimiminika)
Namna magonjwa ya kuhara yanavyosambazwa

Zoezi hili litasaidia kuonyesha jinsi vijidudu vinavyosababisha kuharisha vinavyosafiri kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Watu watachora michoro na kuiunganisha ili kupata kisa kizima.

Muda: saa 1.00 hadi saa 1.30

Vitu muhimu: Karatasi ndogo ya kuchorea, karatasi kubwa ya kuchorea, kalamu za rangi au kalamu kubwa, gundi, na sampuli ya michoro.

examples of drawings; dirty hands and feet, plate of food covered with flies, man defecating, woman washing plate in stream, and person eating.
  1. Unda makundi ya watu 5 hadi 8. Kila mtu achore picha ambayo anafikiri inaonyesha njia moja au nyingine watu wanavyopata magonjwa ya kuhara. Kila mchoro uonyeshe sehemu moja tu ya hadithi nzima ya jinsi ugonjwa wa kuhara unavyosambazwa. Kama mtu hawezi kuchora, anaweza kuandika neno tu au kupata msaada kutoka kwa mtu mwingine. Kuwepo sampuli za michoro husaidia kuchochea majadiliano katika makundi.
  2. Kila mtu aonyeshe mchoro wake katika kundi lake dogo. Watu wengine katika kundi waseme ni nini wanachoona. Hii ni kumwezesha kila mtu kuielewa michoro.
  3. Kila kundi liweke michoro yake katika mpangilio ambao unaonyesha hadithi kuhusu namna vijidudu vya magonjwa vinavyoenea. Iwapo kundi litaona kuna michoro ambayo inakosekana, kundi litaandaa michoro mipya inayofaa kujaza mapengo hayo katika hadithi husika. Pale michoro inapokuwa katika mpangilio unaofaa, ibandikwe kwenye karatasi kubwa. Chora mishale kati ya michoro ili kutengeneza kielelezo cha namna vijidudu vya magonjwa vinavyoenea.
  4. Kila kundi lioneshe kielelezo chake kwa makundi mengine. Kundi lielezee jinsi ugonjwa wa kuharisha unavyoenea kutoka mtu mmoja hadi mwingine.
  5. Washiriki katika makundi yote hatimaye wafanye majadiliano ya pamoja juu ya zoezi zima. Je, hadithi za makundi yote zinafanana? Je, kuna tofauti zipi katika hadithi za makundi hayo? Kwa nini? Zungumzia njia mbalimbali ambazo hueneza ugonjwa wa kuhara. Ni kwa namna gani hali za kiuchumi na kijamii huwaweka watu katika hatari? Ni tabia na imani zipi ambazo huwaweka watu hatarini? Ni njia gani nyingine za uenezaji ambazo hazikuonyeshwa katika zoezi hili?

Magonjwa ya kuhara

crouching child having diarrhea. Magonjwa mengi ya kuhara husababishwa na ukosefu wa maji kwa ajili ya kufanyia usafi binafsi, vyoo visivyo safi na salama, pamoja na maji na vyakula ambavyo vimechafuliwa.

Dalili

Dalili kuu ya ugonjwa wa kuhara ni mharo au kinyesi chenye maji maji kila baada ya muda mfupi. Dalili nyingine ni pamoja na homa, kuumwa kichwa, kutetemeka, kujisikia baridi, udhaifu wa mwili, maumivu ndani ya tumbo, kutapika na tumbo kuvimba. Aina ya matibabu kwa mgonjwa hutegemea ugonjwa gani wa kuhara mtu alio nao. Dalili hizi zinaweza kusaidia kubainisha aina ya ugonjwa wa kuhara mtu alio nao:

  • Kipindupindu: kuhara kinyesi kinachofanana na maji yaliotumika kuoshea mchele, maumivu na usokotaji tumboni, na kutapika.
  • Homa ya matumbo (taifodi): homa, maumivu makali na usokotaji tumboni, maumivu ya kichwa, shida katika kutoa kinyesi au mharo mzito.
  • Giardia: mharo ambao unaonekana kuchanganyika na mafuta ya grisi, wenye vitu vinavyoelea na kutoa harufu mbaya, maumivu ya tumbo, homa kiasi, kutapika, gesi tumboni, na kucheua hewa yenye harufu kama ya mayai yaliyochemshwa.
  • Kuhara damu: mharo uliochanganyika na damu mara 4 hadi 10 kwa siku, homa, maumivu makali na usokotaji tumboni.
  • Kuhara kinyesi kilichochanganyika na kamasi (Ameba): kuharisha mara 4 hadi 10 kwa siku, mara nyingi kinyesi kikiwa na kamasi, homa, maumivu makali na usokotaji tumboni, na kuharisha mara baada ya kula.
  • Minyoo: tumbo lililovimba, kuharisha, udhaifu, minyoo ambayo inaweza kuonekana kwenye kinyesi, au kutoka kupitia mdomoni na puani, upungufu wa damu mwilini - anemia, na ngozi kupauka.


Magonjwa ya kuhara na upungufu wa maji mwilini
EHB Ch5 Page 52-1.png

Watu wengi hufariki kutokana na magonjwa ya kuhara, hasa watoto. Mara nyingi watoto hufariki kwa sababu ya kupungukiwa maji mwilini. Watu wa umri wote wanaweza kukabiliwa na upungufu wa maji mwilini. Lakini upungufu mkubwa wa maji mwilini hujitokeza haraka sana kwa watoto wadogo na ni hatari sana kwao.

Mtoto yeyote anayeharisha yuko katika hatari ya kupungukiwa maji mwilini. Mpatie vinywaji kwa wingi na kumpeleka haraka kwenye kituo cha afya mara moja.

EHB Ch5 Page 52-2.png
Dalili za kupungukiwa maji mwilini
Utosi kurudi ndani
Macho kurudi ndani na kutoa machozi
Kusikia kiu na midomo kukauka
Kupungua uzito haraka
Kukosa mkojo au kutoa mkojo kidogo au wenye rangi ya njano iliyokolea
Ngozi ya mwili ikivutika hairudi katika hali yake ya kawaida
Vuta ngozi na vidole vyako
Ngozi isiporudi katika hali yake ya kawaida mtoto amepungukiwa maji mwilini
Kuzuia upungufu wa maji mwilini

Mtoto anapoanza kuharisha na kutapika, usisubiri dalili za upungufu wa maji mwilini. Chukua hatua za haraka:

  • Mpe vinywaji kwa wingi, kama vile uji mwepesi, mchuzi, maji, au kinywaji maalum cha kuongeza maji mwilini (tazama ukurasa unaofuata).
  • Endelea kumpa chakula. Mtoto (au mtu mzima) ambaye ni mgonjwa anapoweza kula, mpatie chakula anachopenda kila baada ya muda mfupi. Kwa watoto, endelea kunyonyesha maziwa ya mama kwa kuzingatia ushauri wa mtaalam wa afya, kabla ya kuwapa vyakula au vinywaji vingine.
  • Kinywaji maalum cha kuongeza maji mwilini husaidia kuzuia upungufu wa maji mwilini. Kinywaji hiki hakiponyeshi ugonjwa wa kuharisha, lakini kinaweza kumsaidia mgonjwa mpaka kuharisha kutakapokoma.
Jinsi ya kutengeneza kinywaji maalum cha kuongeza maji mwilini

Hapa kuna njia mbili za kutengeneza kinywaji cha kuongeza maji mwilini. Kama inawezekana, ongeza kwenye kinywaji hicho nusu kikombe cha juisi ya matunda, maji ya madafu au ndizi zilizopondwapondwa. Hivi vyote vina madini ya potasiamu, ambayo humsaidia mgonjwa kula chakula na kunywa zaidi.

Mpe mtoto kinywaji hiki kidogo kidogo kila baada ya dakika 5, usiku na mchana, hadi atakapoanza kukojoa kama kawaida. Mtu mzima anahitaji lita 3 au zaidi za kinywaji kwa siku. Mtoto mdogo anahitaji angalau lita 1 kwa siku, au glasi moja kwa kila mharo. Endelea kumpa mgonjwa kinywaji hiki kadri inavyohitajika. Hata kama mgonjwa anatapika, siyo rahisi kutapika kinywaji chote alichokunywa. Baada ya siku moja, mwaga kinywaji kilichobaki na kutengeneza kingine iwapo bado kinahitajika.


Kilichotengenezwa kwa unga wa nafaka na chumvi

(Mchele uliosagwa ni bora zaidi: Lakini unaweza kutumia unga wa mahindi, ngano, ulezi au nazi vilivyopikwa na kupondwapondwa.)

WWHND ChSk Page 540-2.png
WWHND ChSk Page 540-3.png
Katika lita 1 ya MAJI safi tia CHUMVI nusu ya kijiko cha chai,


Na vijiko 8 vya chai vilivyojazwa vizuri unga wa NAFAKA.
EHB Ch5 Page 53-5.png


Chemsha kwa dakika 5 hadi 7 ili kutengeneza uji mwepesi. Poza kinywaji hicho haraka na anza kumpa mgonjwa.

TAHADHARI! Onja kinywaji kila wakati kabla ya kumpa mgonjwa ili kuhakikisha kwamba hakijaharibika. Vinywaji vya nafaka vinaweza kuharibika ndani ya saa chache katika hali ya joto.

Kilichotengenezwa kwa sukari na chumvi

(Unaweza kutumia maji ya miwa au sukari)

WWHND ChSk Page 540-3.png
WWHND ChSk Page 540-2.png
Katika lita 1 ya MAJI safi tia CHUMVI nusu kijiko cha chai,

Na vijiko 8 vya SUKARI, changanya vizuri.
EHB Ch5 Page 53-4.png
TAHADHARI! Kabla ya kuongeza sukari onja kinywaji na kuhakikisha kina chumvi kidogo.

MUHIMU! Iwapo upungufu wa maji mwilini utaendelea au mgonjwa kuonyesha dalili za hatari, tafuta msaada wa daktari
Kusimamisha ueneaji wa kuharisha

Zoezi hili linatumia hadithi kutoka kwenye zoezi “Namna magonjwa ya kuharisha yanavyosambazwa”: Zoezi hili linalenga kuelezea namna ya kuzuia ueneaji wa ugonjwa wa kuhara.
Muda: Dakika 30 hadi 60
Vifaa: Karatasi kubwa ya kuchorea, kalamu za rangi au kalamu za wino mzito, gundi ya karatasi, picha kutoka kwenye jaribio “Namna magonjwa ya kuhara yanavyoenezwa”:

EHB Ch5 Page 54-1.png
  1. Rudi katika makundi madogo yaliyotumika wakati wa zoezi la “Namna magonjwa ya kuhara yanavyoenezwa”, na kila kikundi kiangalie picha kutokana na zoezi hilo la awali. Kila kikundi kijadili jinsi ya kuzuia ugonjwa huo kwa kunawa mikono, kutumia vyoo, utunzaji vizuri wa chakula na maji, na kwa njia zingine zinazofaa. Kila moja ya hatua hizi huzuia ueneaji wa magonjwa ya kuhara.
  2. Baada ya kila kikundi kukubaliana juu ya njia bora za kuzuia kusambaa kwa vijidudu vya magonjwa, kikundi kichore picha kuonyesha njia tofauti za kusimamisha magonjwa ya kuhara.
  3. Kila kikundi kijadili jinsi ya kubadili hadithi kutoka jinsi magonjwa ya kuhara yanavyosambazwa kuwa jinsi ya kusimamisha kuenea kwa magonjwa ya kuhara. Je picha hizo zitaingia katika nafasi gani ndani ya hadithi hiyo ili kusimamisha magonjwa ya kuhara? Picha hizo zibandikwe katika hadithi ya awali na kuonyesha jinsi hadithi itakavyobadilika.
  4. Kila kikundi kionyeshe hadithi yao mpya. Yafanyike majadiliano ya pamoja juu ya njia za uzuiaji watakazotumia na zipi hawatatumia na kwa nini. Je njia zote za uzuiaji zilizopendekezwa zinaweza kufanya kazi wakati wote? Kwa nini zifanye kazi au kwa nini zisifanye kazi? Kwa nini ni vigumu kutumia baadhi ya njia hizi? Ni kwa namna gani jamii inaweza kufanya kazi pamoja ili kuhakikisha kwamba magonjwa ya kuhara yanadhibitiwa?
Sw EHB Ch5 Page 54-2.png

Minyoo aina ya Guinea

Minyoo ya Guinea ni mirefu, myembamba sana, huishi chini ya ngozi na husababisha kidonda chenye maumivu kwenye mwili. Mnyoo huu ambao huonekana kama uzi mweupe unaweza kukua na kufikia urefu wa mita 1. Minyoo ya Guinea hupatikana katika sehemu za Afrika, India na Mashariki ya Kati.

Dalili

Uvimbe wenye maumivu hujitokeza katika kifundo, mguuni, au sehemu yoyote ya mwili. Baada ya siku chache au wiki, jipu hujitokeza ambalo baadae hupasuka na kuacha kidonda. Jambo hili mara nyingi hutokea mtu anapokuwa amesimama kwenye maji au anaoga. Kichwa cha mnyoo huu wa Guinea unaofanana na uzi mweupe hujitokeza na kinaweza kuonekana kwenye kidonda. Mnyoo huu huweza kujivuta na kujitoa nje ya mwili wa mgonjwa katika wiki inayofuata. Iwapo kidonda kitaingiwa na uchafu na maambukizi mengine, au mnyoo unapokatikia ndani wakati wa kuuvuta ili kuutoa nje, maumivu na uvimbe husambaa, na mgonjwa anaweza kupata shida sana kutembea.

Minyoo ya Guinea inaenezwaje?

Minyoo hii huenezwa kutoka mtu mmoja hadi mwingine kwa njia zifuatazo:

EHB Ch5 Page 55-1.png

1. Mtu aliyeambukizwa ambaye ana kidonda anapokanyaga kwenye kisima, bwawa, mto au chanzo cha maji, mnyoo wa Guinea hutoa sehemu yake nje ya kidonda na kutaga mayai kwenye maji.
2. Wadudu wadogo wa majini hula mayai ya minyoo hiyo.
3. Mtu mwingine hunywa maji kutoka chanzo hicho na kumeza wadudu na mayai ya minyoo yaliyoko kwenye maji.
4. Baadhi ya mayai hukua na kuwa minyoo chini ya ngozi. Baada ya mwaka mmoja, kidonda hutokea pale minyoo inapovunja ngozi ili kutaga mayai nje.
Kudhibiti maambukizi ya minyoo ya Guinea

Linda vyanzo vya maji na chuja maji. Iwapo hakuna mtu anayekanyaga au kuoga kwenye maji yanayotumika kwa ajili ya kunywa, maambukizi ya minyoo ya Guinea hayataenea na hatimaye ugonjwa huu utatoweka katika eneo husika.

Minyoo ya kwenye damu

Minyoo ya kwenye damu ni pamoja na kichocho, schistosomiasis, na snail fever. Minyoo huingia kwenye damu kupitia ngozi baada ya mtu kupita, kuoga au kuogelea kwenye maji yenye minyoo hiyo. Maambukizi hayo yanaweza kusababisha madhara makubwa kwenye ini na figo, na hata kifo baada ya miezi au miaka kadhaa. Wanawake wapo katika hatari kubwa ya kuambukizwa minyoo ya damu kwa sababu hutumia muda mwingi kwenye maji au wakishughulika na maji, mathalan kuchota, kuyatumia kufua nguo, kuwaogesha watoto, kulima na kumwagilia bustani, katika mashamba ya mpunga nk.

Wakati mwingine, maambukizi hayo hayaoneshi dalili mapema. Dalili ya kawaida katika baadhi ya sehemu ni kutoa mkojo au kinyesi kilichochanganyika na damu. Huweza pia kusababisha vidonda sehemu za ukeni kwa wanawake. Katika maeneo yenye hatari kutokana na ugonjwa huu, hata watu walio na dalili ndogo sana au maumivu ya tumbo wanapaswa kuwahi kwenye kituo cha kutolea huduma za afya na kupata ushauri.

Sw EHB Ch5 Page 56-1.png

Minyoo ya kwenye damu huenezwa hivi:

1. Mtu aliyeambukizwa anakojoa au kujisaidia kinyesi kwenye maji.
2. Mkojo au kinyesi kina mayai ya minyoo hiyo ndani yake.
3. Mayai huangua na kuingia kwenye konokono wadogo.
4. Minyoo michanga hutoka kwa konokono na kumwingia mtu mwingine.
5. Kwa njia hii, yeyote ambaye anaoga, kufulia au kuogelea ndani ya maji hayo anapata maambukizi.
Matibabu

Minyoo ya kwenye damu inaweza kutibiwa na kupona. Hivyo, kila mwenye dalili za maambukizi hayo anashauriwa kuwahi kwenye kituo cha kutolea huduma za afya.

Kudhibiti maambukizi ya minyoo ya damu

Minyoo ya kwenye damu haienezwi moja kwa moja kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Kwa sehemu ya maisha yao, minyoo ya kwenye damu lazima iishi ndani ya aina fulani ya konokono wa majini. Hivyo, konokono hawa wakitokomezwa minyoo ya damu itadhibitiwa. Hata hivyo, njia muhimu zaidi ya kudhibiti maambukizi hayo ni elimu na kanuni za afya kwa jamii zinazohimiza kuacha kukojoa, kujisaidia au kutupa vinyesi ndani au karibu na maji.


Ukurasa huu ulihuishwa: 04 Juni 2022