Hesperian Health Guides

Uharibifu wa misitu

Katika sura hii:

Misitu mingi huharibiwa na kampuni za magogo na mashirika mengine yanayonufaika kutokana na matumizi ya rasilimali za misitu yasiyoendelevu. Msitu mmoja unapoangamizwa, kampuni hizo kubwa huhamia kwenye msitu mwingine. Lakini watu wanaoishi ndani au karibu na msitu huo ulioangamizwa kawaida hawana pa kwenda.

Watu wasiotegemea misitu moja kwa moja bado wanatumia mazao mengi yanayotokana na misitu kama vile vitabu na magazeti, vifaa vya ujenzi, chakula kama nyama, soya, mafuta ya mawese, na madini yanayochimbwa chini ya misitu. Ni mara chache watu kufikiria kupanda upya misitu iliyoharibiwa kwa njia hizi.

Jinsi misitu inavyoharibiwa na kuangamizwa

Iwapo rasilimali za misitu hazitatumika na kusimamiwa kwa njia ambazo zinaruhusu misitu kuendelea kukua na kuzalisha, karibu misitu yetu yote itapotea. Sababu za uharibifu mkubwa wa misitu ni pamoja na:

  • Ukataji wa miti yote katika eneo moja kwa ajili ya magogo au upasuaji mbao: Hali hii husababisha mgandamano na mmomonyoko wa ardhi, uharibifu wa maisha ya viumbehai vya porini na kujaza uchafu kwenye mito na njia zingine za maji .
  • Kilimo cha mashamba makubwa: Ufugaji wa ng’ombe wengi na mashamba ya miti mara nyingi huhusisha ufyekaji wa misitu ili kupata ardhi inayohitajika kwa ajili ya mashamba hayo.
  • Mashamba ya kamba maeneo ya pwani: Mashamba hayo huanzishwa kwanza kwa kusafisha maeneo oevu yenye mikoko na misitu mingine ya pwani. Hali hii husababisha jamii ndogo za wavuvi kukosa riziki, uchafuzi wa maji, ongezeko la magonjwa, umaskini na utapiamlo.
  • Viwanda vya kutengeneza karatasi: Huzalisha taka zenye sumu ambazo huchafua ardhi, maji na hewa.
  • Miradi ya ujenzi wa mabwawa makubwa: Husababisha maeneo makubwa ya misitu kufunikwa na maji. Watu hulazimika kuhama kutoka eneo la mafuriko na kukata miti ili kutengeneza makazi mapya na mashamba.
  • Kampuni za uchimbaji madini, mafuta na Gesi: Hukata miti na kuzalisha taka zenye sumu ambazo huchafua maji, ardhi na hewa.
A fat man with a money sign on his pocket stands in a landscape of tree stumps in front of piles of timber and a smoky factory.
Mashirika ya kibiashara na serikali mara chache huzingatia afya na riziki za watu pale misitu inapogeuzwa kuwa bidhaa ya kuuzwa na kununuliwa




Ukurasa huu ulihuishwa: 04 Juni 2022