Hesperian Health Guides

Matibabu bora zaidi ni yapi?

Katika sura hii:

Je, tiba inasaidia au inaathiri afya zaidi?

Ingawa Petro alikuwa na uhakika kwamba dawa zingeponya tatizo hilo, Juanita alihitaji taarifa zaidi kabla ya kuamua kuhusu matibabu haya. Kwa mfano, alijua kwamba tiba ya asili mara nyingi ilikuwa ikimsaidia mama yake na bibi yake walipokuwa wanaugua. Kwa nini sasa tiba ya asili aliyokuwa ametumia haikumsaidia? Yafuatayo ni maelezo ya Petro:

Don Pedro speaking to Juanita
Kila jamii imebuni tiba zake za asili za kutatua matatizo ya afya. Tiba za asili na dawa za kisasa zinaweza kwa pamoja kusaidia sana iwapo zitatumika kwa uangalifu na kwa usahihi. Lakini kumbuka kwamba vyote viwili, tiba za asili na dawa za kisasa, zinaweza kusaidia, kutosaidia chochote, au kudhuru afya zaidi.

Kwa upande wa suala la Juanita, tayari alikuwa ametumia aina zote tatu za tiba:

an ear of corn next to a cup of tea

Chai ya mbelewele za mahindi ingeweza kumsaidia iwapo angekuwa na maambukizo kwenye njia ya mkojo. Hii ni kwa sababu chai ya mbelewele za mahindi humfanya mtu akojoe zaidi na hivyo mkojo husaidia kutoa vijidudu nje ya mwili. Lakini chai hii haikumsaidia Juanita kwa sababu maambukizo yake hayakuwa kwenye njia ya mkojo.

a woman with a medicine pouch tied around her waist under her dress

Kufunga kitambaa chenye dawa za asili kuzunguka tumbo ni tiba isiyo na madhara. Hii haitazidisha tatizo husika lakini pia haitasaidia kitu.

a woman putting plant medicines into her vagina

Kuingiza dawa za mitishamba ukeni ni hatari sana na kamwe haipaswi kufanyika. Dawa za mitishamba zinaweza kusababisha muwasho na mchubuko ukeni na hivyo kurahihisha maambukizo hatari.

Petro alimwambia Juanita angeweza kujifunza kuhusu tiba mmoja moja na jinsi inavyofanya kazi kwa kuongea na watu tofauti waliowahi kuitumia tiba hiyo. Yafuatayo ni maswali ya kuuliza:

  • Kwa nini unatumia tiba hii ?
  • Wakati gani unapaswa kuitumia?
  • Unaitumiaje?
  • Ni kitu gani kinatokea unapoitumia?
  • Ina ufanisi wa kiasi gani?
  • Je, ina madhara yoyote?

Fikiria kwa makini kuhusu wasemavyo watu tofauti juu ya tiba waliyotumia. Kisha, wakati utakapojaribu kutumi tiba hiyo, angalia kwa makini ni kitu gani kitatokea kwenye dalili zako ili ujue iwapo tiba inakusaidia au la. Kuwa mwangalifu kutotumia aina nyingi za tiba kwa wakati mmoja.

a woman offering a medicine pouch to Juanita

Hii ilimsaidia Maria, inaweza kukusaidia wewe pia.
Lakini Maria alikuwa na maumivu baada ya kujifungua, na sio wakati wa kukojoa. Hivyo tiba hii huenda isinisaidie hata kidogo.
chupa za vidonge
Juanita aliporidhika kwamba dawa za kisasa ndio tiba bora kwa matatizo yake ya afya, Petro alimpa vidonge viitwavyo, "doxycycline" na "cotrimoxazole" na kumwambia arudi baada ya wiki moja, baada ya kuvitumia vyote. Pia alimweleza kwamba mumewe, ambaye alikuwa mbali tayari, anapaswa pia kutibiwa kwa dawa hizo mara atakaporudi, na kwamba ni lazima waanze kutumia kinga wakati wa kufanya ngono.


Juanita aliporudi kumwona Petro wiki iliyofuata, alimwambia kwamba tayari amekwisha tumia vidonge vyote alivyompa lakini dalili zake zilikuwa bado hazijaondoka. Pia tatizo la kutokwa majimaji lilikuwa limezidi na rangi yake kugeuka ya njano. Petro aliamua kumuomba msaada Valeria, ambaye ni mtabibu mwenye ujuzi zaidi.

mtabibu Valeria akiongea na Juanita

Valeria alikubali kwamba Juanita alikuwa na ugonjwa wa ngono. Lakini kwa vile dawa alizopewa zilikuwa hazijamsaidia, alihisi kwamba huenda akawa na aina ya kisonono ambayo ina usugu na dawa ya "co-trimoxazole". Valeria alieleza kwamba aina nyingi za kisonono sugu, zimeletwa na maaskari wa kigeni kwenye kambi za jeshi huko Pwani, ambao wamekuwa wakiwaambukiza wanawake wenyeji wakati wanapofanya nao ngono. Valeria alishauri Juanita aende jijini ambapo ataweza kupata uchunguzi zaidi na kupimwa kisonono, kaswende na saratani. Pia huko jijini angeweza kupatiwa dawa mpya na zenye ufanisi zaidi iwapo itahitajika.

Hatari zilizopo na faida

Juanita alikwenda nyumbani akifikiria la kufanya. Angelazimika kutumia kiasi kikubwa cha akiba ya familia ili kugharamia safari ya kwenda jijini pamoja na dawa. Kwa vile safiri ingechukuwa siku mbili (saa 6 kwa basi na kutembea — kwa kwenda na kurudi), na mumewe bado alikuwa mbali huko pwani, angepaswa kumtafuta mtu wa kumwangalizia watoto atakapokuwa hayupo.

Juanita alihofia mumewe angekasirika iwapo angerudi nyumbani na kugundua kwamba ametumia kiasi kikubwa cha fedha kwenda kumwona daktari. Lakini pia alikuwa na hofu kwamba kama asingekwenda kumwona daktari hali yake ingezidi kuwa mbaya zaidi. Valeria alimwambia kwamba bila kutibiwa angeweza kumwambukiza mtoto iwapo angebeba mimba. Baada ya muda pia angeshindwa kupata watoto, na ingesababisha maumivu makali chini ya tumbo, na matatizo kwenye njia ya mkojo na wakati wa hedhi. Mumewe pia angeweza kupata matatizo makubwa ya afya.

Juanita alijikuta njia panda bila kujua la kufanya, hivyo alikwenda kumwona Valeria tena. Juanita alipoelezea hofu yake, Valeria alimshauri alifikirie tatizo lake kwa njia ifuatayo:

Juanita thinking and then telling the health worker her decision
Hizi ndizo faida za kwenda jijini:
  • Nitapata nafuu na hivyo kuendelea kuihudumia familia yangu.
  • Nitaweza kupata watoto zaidi.
  • Sitamwambukiza mtoto iwapo nitabeba mimba.
Nitakumbana na hatari zifuatazo iwapo nitakwenda jijini:
  • Mume wangu atakasirika mara atakapogundua.
  • Itabidi nitumie sehemu ya akiba yetu
Kama ningeweza kupata nafuu na kuepuka hatari hizi, basi hayo matibabu ya jijini yasingehitajika. Lakini kama ugonjwa huu utazidi na siwezi kupata watoto tena, basi ninapaswa kwenda jijini.
basi ikielekea jijini

Hatimaye, Juanita alikwenda jijini kwa ajili ya matibabu. Madaktari walisema ni kweli kwamba Juanita alikuwa na kisonono na klamidia, na hakuwa na dalili za magonjwa mengine ya ngono. Walimweleza kwamba dawa aliyotumia ilikuwa haifanyi kazi tena katika nchi hiyo kutokana na usugu wa magonjwa hayo kwa dawa hiyo. Hivyo walimpatia dawa mpya kwa ajili yake na mume wake.


Ukurasa huu ulihuishwa: 03 Apr 2023