Hesperian Health Guides
Vitamini na dawa za kuongeza madini mwilini
HealthWiki > Toleo Jipya: Mahali Pasipo na Daktari > Ujauzito na kujifungua > Vitamini na dawa za kuongeza madini mwilini
Chuma, ferasi salfeti, au glukoneti salfeti
Ferasi salfeti husaidia sana katika kutibu au kuzuia matukio mengi ya anemia. Tiba kwa kutumia ferasi salfeti kwa njia ya mdomo kawaida huchukua takriban miezi 3.
Madini ya chuma kawaida hufanya kazi vizuri zaidi yanapotumika pamoja na vitamini C (aidha kwa kula matunda na mbogamboga, au kutumia kidoge cha vitamini C).
Madini ya chuma mara nyingi huvuruga tumbo na ni bora zaidi kutumia dawa hii na chakula. Pia, yanaweza kusababisha ugumu wa choo au choo kufunga hasa kwa watu wenye umri mkubwa, na kufanya kinyesi kuwa na rangi nyeusi. Angalia ushauri juu ya tumbo kufunga.
Matumizi makubwa ya madini ya chuma yaliyo katika mfumo wa majimaji huyafanya meno kuwa na rangi nyeusi. Unaweza kunywa kwa kutumia mrija na kupiga mswaki baadaye.
Kuwa na uhakika kwamba dozi ni sahihi. Ferasi salfeti ikizidi ni sumu. Usitoe madini ya chuma kwa watu ambao wameathirika kutokana na lishe duni. Subiri hadi afya zao zitakaporudi.
Aina tofauti za madini chuma yamekolezwa kwa viwango tofauti na madini hayo. Kwa mfano, kidonge cha miligramu 300 za ferasi salfeti kina ndani yake miligramu 60 ya chuma. Lakini kidonge cha miligramu 325 cha ferasi glukoneti kina miligramu 36 za chuma. Hivyo soma maelezo kwenye kifungashio cha vidonge, chupa ya dawa ya majimaji (sirapu), au vya dawa zingine za kuongeza madini ya chuma kujua kiwango cha chuma kilichomo ndani.
KUZUIA ANEMIA miongoni mwa akinamama wajawazitoKUTIBU mtu ambaye tayari ana ugonjwa wa anemia
DOZI YA FERASI SALFETI KWA MIAKA | |||
KUNDI LA UMRI | KIASI GANI KWA DOZI | VIDONGE VYA 300 MG VINGAPI | KIASI GANI KWA UJUMLA CHA MADINI YA CHUMA |
Chini ya miaka 2 | Mg 125 za ferasi salfet | Tumia madini ya chuma yenye mfumo wa majimaji (sirapu) au saga takriban ¼ kidonge cha mg 300 cha ferasi salfeti kwenye maziwa ya mama | Toa kiasi cha kutosha kukidhi mg 25 za chuma |
Miaka 2 hadi 12 | Mg 300 ya ferasi salfeti | Kidonge 1 cha Mg 300 za ferasi salfeti | Toa kiasi cha kutosha kukidhi Mg 60 za chuma |
Zaidi ya miaka 12 | Mg 600 za ferasi salfeti | Vidonge 2 vya mg 300 za ferasi salfeti | Toa vya kutosha kukidhi kiwango cha mg120 za madini ya chuma |
Asidi ya foliki au foleti
Asidi ya foliki ni vitamini muhimu ambayo husaidia ukuaji na afya ya mtoto katik wiki za mwanzo za ujauzito.
Asidi ya foliki na dawa za kuongeza madini ya chuma mwilini zikitolewa kwa mama mjamzito kwa pamoja huwa na matokeo mazuri zaidi kuliko kutoa kila dawa peke yake. Hata zikitolewa pamoja au kila dawa peke yake, dozi inabaki ile ile.
Ni bora zaidi kuanza kutumia asidi ya foliki kabla hujawa mjamzito ili mwili wako uwe na kiwango cha kutosha kukidhi mahitaji ya mtoto katika zile wiki za mwanzo. Endelea kuitumia katika kipindi chote cha miezi 3 ya ujauzito. Mpe mikrogramu 400 hadi 500 kila siku.