Hesperian Health Guides

Ueneaji wa sumu ya vimelea kwenye damu (sepsisi)

Katika sura hii:

Hali hii hutokea pale maambukizi yanapoenea hadi kwenye mfumo wa damu. Ni hali ya hatari kwa sababu huweza kusababisha mshituko. Kama unafikiri sumu ya ambukizo imeanza kuenea kwenye damu, tafuta msaada wa kitabibu haraka na mgonjwa atibiwe wakati mkiwa njiani.

NWTND fa Page 19-1.png
Dalili za ueneaji wa sumu ya vimelea kwenye damu (sepsisi)
  • Homa au kiwango cha joto la mwili kinashuka chini sana
  • Mapigo ya moyo yanakwenda haraka — mapigo ya moyo zaidi ya 90 kwa dakika.
  • Kupumua haraka — zaidi ya pumzi 20 kwa dakika
  • Kupumua kwa shida
  • Ngozi ya mwili kupauka au kuweka alama
  • Kutoa mkojo kidogo
  • Kuchanganyikiwa au kupoteza ufahamu
  • Shinikizo la damu kwenda chini ya kiwango kinachohitajika


Dalili muhimu zaidi ni homa au kushuka sana kwa kiwango cha joto la mwili, mapigo ya haraka ya moyo, na kupumua haraka. Kama mtu ana dalili kama hizi 2 au zaidi, mpe tiba dhidi ya ueneaji wa sumu kwenye damu (sepsisi).

Matibabu

Tafuta msaada wa kitabibu. Ukiwa njiani:

  • Angalia iwapo kuna dalili zozote za mshituko na kutoa matibabu.
  • Mpe seftriaksoni (ceftriaxone), AU sipro (ciprofloxacin) pamoja na klindamaisini (clindamycin).
  • Safisha vidonda vyote ambavyo vimepata maambukizi, ondoa ngozi iliyokufa, na kamua majipu na vimbe ili kutoa usaha. Kujifunza zaidi juu ya kukamua jipu, angalia Matatizo ya ngozi, kucha, na nywele (inaandaliwa).
  • Kama mgonjwa anapumua vizuri, mpe vinywaji. Mpe kidogo baada ya kila muda mfupi.